04/05/2009

Neno kwenu Mafisadi; Shairi

Jambo jema linofaa lisaidie jamii,
Lijenge mustakabali,na watu walikubali,
Likubalike kwa aali,wa nyumbani na wambali,
Mjionapo si wakweli,achieni ngazi mthaminiwe.

Mfano huu ni kweli, viongozi mafisadi,
Ardhi na rasilimali,hudhulumu kwa ahadi,
Miaka mitano si mbali,wazidi fanya kusudi,
Mjionapo si wakweli achieni ngazi mthaminiwe.

Walisema wanaweza, waliweza kutuibia,
Wakajilia pweza,na nje ya nchi kukimbia,
Huku tumetelekezwa,zatushinda familia,
Mjionapo si wakweli, achieni ngazi mthaminiwe.

Watu waliwazomea, kila wapitapo,
Wakajinadi kwa mazoea,na aibu ingalipo,
Na wapo walolowea, nje ya nchi ndipo walipo,
Mjionapo si wakweli achieni ngazi mthaminiwe.

Ujumbe huno ni wenu, viongozi mafisadi,
Mkiwacha kazi kwenu,nimenena pasi kedi,
Bali jueni ni dhima yenu,kutekeleza ahadi,
Mjionapo si wakweli, achieni ngazi mthaminiwe.

Mtunzi: Kamarade Rashidi Mkwinda (http://www.mkwinda.blogspot.com)

 

2 comments:

  1. kazi kwelikweli dunia hii ya leo

    ReplyDelete
  2. Bora waachie madaraka,lakini wamedondoka kwenye penzi tamu na madaraka na hilo ndo tatizo.

    ReplyDelete