05/10/2011

Makala ya Mdau Emmanuely Deodath Lyimo


“Nguvu za masikini mtaji wa matajiri….masikini hana mtaji”

Na. Emmanuely Deodath Lyimo

“Mtaji wa masikini ni nguvu zake” kati ya semi maarufu za lugha ya Kiswahili. Lakini nimewahi kujiuliza upi mtaji wa tajiri?. Hii inatokana na wasiwasi niliokuwa nao kama kweli masikini hufaidika kadiri ya nguvu anazotumia katika kuzalisha. Kabla sijafika mbali ni muhimu kujiuliza hivi mtaji ni nini? Kadiri nijuavyo mimi mtaji ni mzunguko wa fedha na rasilimali ambazo zinawekezwa katika kuzalisha faida, kwa maana hii fedha zilizoko mfukoni au benki bila ya kuwa katika mzunguko wa kuzalisha faida haziwezi kuwa mtaji. 

Katika mfumo wa kibepari, ili kuzalisha faida fedha hutumika kunulia bidhaa kubwa mbili: nguvu kazi na zana za uzalishaji. Nguvu kazi ni ule uwezo wa mfanyakazi kuzalisha bidhaa au huduma, kwa upande mwingine zana za uzalishaji ni mashine, eneo la kufanyia kazi pamoja na malighafi. Hivyo basi nguvu kazi huwa mtaji pale inapotumika katika kuzalisha faida.

Tofauti na wakati wa utumwa ambapo watumwa walikuwa wanamilikiwa kikamilifu, katika mfumo wa kipepari mabepari wamekuwa wakinunua na kumiliki uwezo wa mfanyakazi/nguvu kazi ili kutengeneza faida. Hivyo basi katika mfumo wa kibepari nguvu kazi ni bidhaa ambayo inaweza kuuzwa na kununuliwa.

Kwa maana hii basi, katika mfumo huu wa kibepari ambao ndio unaoongoza uzalishaji wa bidhaa, uuzaji wa bidhaa sokoni, kilimo, siasa na kila Nyanja ya maisha yetu haiwezekani hata kidogo kwa masikini kumiliki hata nguvu kazi yake mwenyewe. Hata ajitahidi kufanya kazi kwa bidii kiasi gani, nguvu zake zitaendelea kuwa mtaji wa mtu mwingine aliyenunua uwezo wake wa kuzalisha mali. 

Ikumbukwe kuwa, nguvu kazi ndiyo bidhaa pekee yenye uwezo wa kuzalisha thamani zaidi wakati wa uzalishaji wa bidhaa kuliko gharama iliyowekezwa awali. Njia pekee ya kupata faida hii ni kwa kumlipa mzalishaji pungufu ya kile anachozalisha, njia hii ya kupata faida inaitwa unyonyaji

Kwa maana hii usemi huu ni sehemu ya propaganda za mabepari kuendelea kutoa matumaini ya ndoto za alinacha kwa masikini ili waendelee kuwanyonya kiulaini. Katika fikra pevu kamwe kisichokuwa chako hakiwezi kuzalisha faida ikawa yako. Badala ya masikini kuzidi kufanya kazi kwa bidii katika mfumo huu wa kibepari ambao hauruhusu wao kutengeneza faida ni lazima wajitahidi kupambana ili kurudishiwa uwezo wa kumiliki nguvu yao kwanza.

Walalahoi wanajukumu la kijikomboa wao na kila kilicho chao, ikiwemo nguvu kazi yao halafu ndipo wanze kuitumia katika kujikomboa kiuchumi. Hapa ninamaanisha kuwa, kabla ya kuamini kuwa mlalahoi anaweza kujiinua kiuchumi kwa kumfanyia bepari kazi kwa bidii lazima akatae kunyonywa. Maana kabla ya fukara kupata kitu kwa kufanya kazi kwa bidii katika mfumo huu wa kibepari, basi bepari atakuwa amepata mara mbili zaidi yake.

Ninamaliza kwa kutoa changamoto kuwa mtaji wa masikini katika mfumo huu wa kibepari ni mtaji wa matajiri wanaowanyonya mafukara ambao ni wakulima na wafanyakazi. Katika mfumo wa kibepari masikini hana mtaji ila ndoto za alinacha zisizo na tija zinazowafaidisha mabepari kila uchwao. Tuamke tuwe na fikra sahihi, tukatae vimisemo vinavyotupa matumaini yasiyofika milele!!!!

2 comments:

  1. Deo, nzuri sana.
    Pamoja na kujaribu kutambua unyonyaji dhidi yetu, bado tunaendelea kufanya kazi. Hii si ndo Marx aliita "false consciousness"?

    Tunatambua kuwa tonanyonya, lakini hatuna hatua ya kudai haki zetu.

    Wafanyakazi wa umma, taasisi binafsi, Civili societies, japo si sana na wengine wote katika industry nchini, tusimame tutee utu wetu, tusipofanya hivyo hakuna atakaye tutea.

    ReplyDelete